Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Luteni mstaafu Abdallah Kihato, akipanda mti katika Ofisi ya Kijiji cha Magoza kama sehemu ya utunzaji wa mazingira pamoja na uzinduzi wa mradi wa Majiko Banifu uliofadhiliwa na Green Voices. 

“NI aibu mwanamke anatoka alfajiri kwenda kutafuta kuni wakati mume amelala, tena ni mateso makubwa kwa wanawake,” ndivyo anavyoanza kueleza Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Luteni mstaafu Abdallah Kihato, wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Magoza.

DC Kihato alisema hayo hivi karibuni alipokuwa anazindua mradi wa Majiko Banifu wa kikundi cha ‘Moto Moto’ unaotekelezwa na wanawake wa kijiji hicho kupitia mradi wa Green Voices.

Mkuu huyo wa Wilaya alisema kwamba, kitendo cha mwanamke kuamka alfajiri kwenda vichakani kutafuta kuni kinaitia doa hata ndoa yenyewe kwa maana kinaongeza mateso kwa upande mmoja hasa mama anapokosa usingizi wa alfajiri.

Alisema mradi huo wa majiko banifu ni wa msingi hasa katika kipindi hiki ambapo mazingira yameharibiwa kutokana na ukataji ovyo wa miti kwa ajili ya mkaa na kuni, hali ambayo inawawia vigumu hata wanawake kupata kuni za kupikia.

Majiko hayo banifu yanajengwa kwa kutumia udongo wa kawaida wa kwenye vichuguu na gharama pekee ni sukari na vibao vya kufyatulia matofali.

“Misitu yote imekatwa, tena wanaume ndio wanaoongoza kwa ukataji wa miti huku wanawake wakiwa ndio waathirika wakubwa.

“Kila siku ukisimama barabarani utaona malori na baiskeli zimebeba mkaa na kuni kupeleka mjini (Dar es Salaam), wanaume wanaona fahari kukata kuni na mkaa kwenda kuuza lakini hawako tayari kutafuta kuni za kupikia nyumbani, ni aibu kubwa,” alisema DC Kihato.

Aidha, alisema kuni bora zinapelekwa kuuzwa mjini Dar es Salaam wakati wanawake wanabaki kuokoteza kuni ndogo ndogo ambazo zinakwisha baada ya muda mfupi, hivyo kulazimika tena kurudi vichakani.
Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Luteni mstaafu Abdallah Kihato, akiwasili katika Kijiji cha Magoza, Kata ya Kiparang’anda kuzindua mradi wa Majiko Banifu uliofadhiliwa na Green Voices ambao unalenga wanawake kupaza sauti zao katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 2 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 24, 2016

    Ni aibu kabisa wanaume ni kujizatiti kuamka mapema kujishughulisha na kutimiza wajibu katika familia.

    ReplyDelete
  2. AnonymousMay 24, 2016

    Wanaume tubadilike. Nyakati pia zimebadilika.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...